Saturday 27 August 2016



Serikali Kushirikisha Wataalamu Kuikwamua Sekta ya Utalii, Ukarimu
Na Vincent Mpepo-OUT
Serikali imesema kuwa itaendelea kushirikisha wataalamu na watafiti katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazoikabili sekta ya Utalii na Ukarimu ili kuibua fursa na bidhaa mpya kupitia sekta hiyo kwa lengo la kuongeza pato la taifa.
Kauli hiyo imetolewa na Meja Jenerali Gaugence Milanzi, Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii wakati akifunga wa Kongamano la Kimataifa la Utalii, Ukarimu na Ubunifu  kwa Nchi zinazoendelea jijini Dar es salaam lililoandaliwa na Idara ya Utalii na Ukarimu ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
Alisema kuwa kongamano hilo limekuwa mwanzo mzuri wa kuwakutanisha wataalamu, watafiti na wadau wa ndani na nje ya nchi ambao kwa pamoja wamejadili changamoto zinazoikabili sekta ya utalii na ukarimu na kushirikishana uzoefu katika kupata suluhisho.
“Kongamano hili liwe mwanzo mzuri wa kuendelea na mijadala mingine kwa siku zijazo kwa lengo la kupata mawazo yatayosaidia kukuza sekta ya utalii”,alisema Meja Jenerali Gaugence Milanzi.
Alisema serikali kwa upande wake itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama kwa kuwa ni kivutio kimojawapo kwa wageni na watalii hivyo kuwataka wananchi kuunga mkono juhudi hizo kwa kuendelea kuwa wakarimu kwa watalii na wageni.
Aidha aliwaasa wananchi kutokuwa na mawazo hasi kwa sheria ya ongezeko la kodi (VAT) katikalinaloigusa sekta ya utalii na ukarimu kwani ina malengo mazuri ya kuongeza mapato ya serikali ambayo yatatumika katika uboreshaji wa huduma za jamii na miundombinu.
“Tujipe muda wa kuona matokeo ya utekelezaji wa sheria hii badala ya kuwa na mawazo hasi kwa sheria hiyo”
Kwa upande wao, waandaji na washiriki wa kongamano hilo wameishauri serikali kuwatumia wataalamu na watafiti hapa nchini katika sekta ya utalii na ukarumu ili mchango wao usaidie kuboresha sekta hiyo katika kukuza uchumi wa nchi.
Akiwasilisha majumisho ya kongamano hilo, Daktari Shogo Mlozi, Mhadhiri na Mkuu Idara ya Utalii na Ukarimu ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania alisema kuwa serikali iwatumie wataalamu na watafiti kutoka hapa nchini katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto katika sekta ya utalii na ukarimu.
“Ni muhimu serikali ikahusisha wataalamu katika uundaji wa sera na miongozo mbalimbali kwani watatoa utalaamu wao kwa manufaa ya Taifa”, alisema Dkt. Mlozi.
Alisema kuwa watafiti na wanataluuma wana nafasi kubwa ya kutoa mchango katika uboreshaji sekta ya utalii kupitia tafiti ambazo zikizingatiwa zinaweza kusaidia katika uboreshaji wa sekta ya utalii hivyo kuiimarisha sekta hii muhimu kwa uchumi wa taifa.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Jamii, Dkt.Felician Mutasa alisema kuwa kuna hazina kubwa ya wataalamu ambao wakishirikishwa wanaweza kutoa mchango katika sekta ya utalii kupitia tafiti, ushauri na uboreshaji wa sera ya utalii kwa manufaa ya nchi.
Profesa Elifas Bisanda, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania alisema kuwa bado kuna changamoto nyingi katika sekta ya utalii lakini zaidi katika ukarimu amabapo watanzania hawajajidhatiti katika utoaji huduma bora kwa watalii na wageni.
Akitolea mfano changamoto wa huduma za hoteli hasa kwa upande wa chakula alisema kuwa si ajabu mgeni anaweza kuambiwa asubiri kwa muda fulani na hatimaye akaambiwa chakula bado hata baada ya muda huo kupita swala linaloitia doa sekta hii ukilinganisha na huduma katika hizohizo katika nchi nyingine.
“Jambo la msingi ni kujitathimini ni kwa namna gani tunawajali wageni na watalii katika utoaji wa huduma”,alisema Profesa Bisanda.
Alisema kuwa kuna umuhimu wa jamii kuelimishwa ili ijue namna ya kuwahudumia na zaidi kuwajali wageni na watalii ili kuwafanya wapende kuja Tanzania na wawe mabalozi wazuri wakirudi nchini kwao.
Kwa miaka ya hivi karibuni takwimu zinaonesha kuwa sekta ya utalii imetoa mchango mkubwa katika pato la taifa wa hadi aslimia zaidi ya 17 na asilimia 25 ya fedha za nje hivyo ni muhuimu serikali ikaipa kipaumbele.
Kongamano hilo la kimataifa katika Utalii na Ukarimu liliandaliwa na Idara ya Utalii na Ukarimu ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikewemo Shirika la Hifadhi la Taifa, Serena Hotels, Leopard Tours Limited, Hyatt Regency na Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha na Kituo cha Mikutano cha Mwlalimu Julius Nyerere.

No comments: